tangazo

Tuesday, January 29, 2013

KUACHIWA KWA LULU: MAMA KANUMBA ALIA ZAIDI YA MASAA MAWILI.

Na Hamida Hassan
HABARI za staa wa sanaa za maigizo nchini, Elizabeth Michael ‘Lulu’, kuachiwa kwa dhamana, zimemkumbusha mbali mama mzazi wa marehemu Steven Kanumba, Flora Mtegoa, hivyo kumfanya aangue kilio kwa saa mbili.
Elizabeth Michael ‘Lulu’ akiwa mahakamani jana.
Mama Kanumba, yupo mkoani Kagera kwa sasa, mara alipozipata taarifa za Lulu kuachiwa huru, alichukua picha yamarehemu Kanumba kisha akajikunyata, akakaa sebuleni peke yake na kuanza kuangua kilio.
Takriban saa moja tangu Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, ilipotangaza kumwachia Lulu kwa dhamana, chanzo chetu mkoani Kagera kilituhabarisha: “Mama Kanumba leo amekuwa mnyonge tofauti na siku zote, aliposikia tu Lulu kaachiwa huru, amejiinamia tu, analia sana.”
Baada ya kupata taarifa hizo, mwandishi wetu alimpigia simu Mama Kanumba ambaye alipopokea tu, kilio kilisikika.
Wakati analia, Mama Kanumba alisema: “Siumii Lulu kuachiwa, najua ni mapenzi ya Mungu ila naumia sana kwa sababu mwanangu mpenzi nilishamzika.”

Mama mzazi wa marehemu Steven Kanumba, Flora Mtegoa.
Hata hivyo, mazungumzo hayo yalikoma baada ya Mama Kanumba kushindwa kunyamaza, licha ya mwandishi wetu kutumia muda mwingi kumbembeleza aache kulia.
Saa moja na nusu baadaye, Mama Kanumba akiwa amenyamaza, alimpigia simu mwandishi wetu, akieleza kwamba pale alipo ameshikilia picha ya Kanumba ambayo inamkumbusha machungu aliyokua ameanza kuyasahau.
AKAZUNGUMZA MAZITO
Kuhusu kile kinachomuuma zaidi, Mama Kanumba alisema: “Anayeniumiza ni Mama Lulu, sisi wote ni wazazi lakini hata siku moja hajaja kuniona, kunipa pole, japo najua kilichotokea siyo mapenzi ya Lulu.”
KUNA WAMBEA WALICHAFUA HALI YA HEWA
Mama Kanumba alisema: “Kuna watu wamenipigia simu huko Dar es Salaam kwamba leo kutakuwa na sherehe ya nguvu ya kumpongeza Lulu kupata dhamana.”
Je, hilo lina ukweli? Staa wa Filamu, Mahsein Awadh ‘Dk. Cheni’ ambaye amekuwa bega kwa bega kuhakikisha Lulu anapata dhamana, alisema: “Hakuna sherehe, hatuwezi kufanya hivyo, jamii haitatuelewa.”
Mama Lulu naye: “Jamani namshukuru Mungu kwa Lulu kupata dhamana, hakuna sherehe. Mazingira ya kesi yalivyo, haitakuwa vizuri kufanya sherehe, haitakuwa ubinadamu.”
MASHITAKA YA LULU
Lulu anakabiliwa na kesi ya kumuua bila kukusudia, aliyekuwa mcheza filamu maarufu Afrika, Steven Kanumba.

No comments:

Translate