tangazo

Sunday, December 30, 2012

CHADEMA YASEMA:SERIKALI NDIO CHANZO CHA MVUTANO WA GESI


NAIBU Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe amesema wananchi wa Mtwara na Lindi wana haki ya kuandamana kuhoji jinsi watakavyonufaika na mradi wa gesi.

Naye, Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Nishati na Madini,
 John Mnyika amesema njia rahisi ya kutatua migogoro ya namna hiyo ni nchi kuwa na sera  ya mfumo wa majimbo.

Desemba 27 mwaka huu maelfu ya wakazi wa Mkoa wa Mtwara waliandamana wakipinga uamuzi wa Serikali kusafirishwa gesi kwa njia ya bomba kutoka mkoani humo kwenda Dar es Salaam.

Katika taarifa iliyotolewa na Zitto jana alisema hoja iliyotolewa na wakazi wa Mtwara ina ukweli ndani yake na inatakiwa kufanyiwa kazi.

“Wananchi hawa hawasemi kwamba gesi na mazao yake vibaki Mtwara na Lindi, wanataka umeme uzalishwe Mtwara usambazwe nchi nzima, mbolea izalishwe Mtwara na kusambazwa nchi nzima, wanataka bandari  ya Mtwara iboreshwe na kuhudumia mikoa ya Kusini, hawasemi mapato yote ya gesi yatumike Mtwara tu” alisema Zitto.

Wakati huo huo, Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika alisema kuwa Waziri wa Nishati na Profesa Sospeter Muhongo amepotosha uma katika kauli aliyoitoa hivi karibuni kwamba sera ya Majimbo ambayo ingeweza kulinda maslahi ya wakazi wa Mtwara haitumiki kokote duniani si sahihi.

Alisema kuwa Profesa Muhongo aliiponda tu kwa sababu ni moja ya sera zilizomo ndani ya katiba ya Chadema lakini si ngeni duniani na imeonyesha manufaa mengi kwa nchi zilizoitumia zikiwepo za Bara la Afrika.

“Suala la sera ya majimbo sio geni duniani.
Nchi kadhaa za Afrika zinafuata mfumo huu mathalani Afrika ya Kusini na Ethiopia,” alisema.

Alitaja faida za sera hiyo kuwa ni kujenga uwezo wa kisiasa, uongozi na uwajibikaji.

Alitoa mfano wa hasara za kutotumia sera hiyo kuwa ni nchi nzima
kuendeshwa na ikulu Dar es salaam hata katika mambo ya madogo nay a kawaida kabisa.

Hali hiyo akaielezea kuwa inachochea urasimu na kuchelewesha mipango ya maendeleo kwa sababu tu uamuzi unatoka ngazi ya juu.

Kuhusu faida alisema: “Sera ya majimbo inaelekeza taifa kuwa na viongozi wa kuchaguliwa moja kwa moja na wananchi katika ngazi mbalimbali.

“Hii ina maanisha kwamba kwa muktadha wa sera ya majimbo ofisi na vyeo vya mkuu wa mkoa, mkuu wa wilaya, katibu tarafa vitafutwa.”

No comments:

Translate