tangazo

Tuesday, October 9, 2012

Bodi Ya Mikopo Zanzibar

Na Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar 9/10/2012 
 
 Jumla ya wanafunzi 800 wa Zanzibar, watafaidika na ufadhili wa masomo ya Elimu ya Juu Kupitia Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu ya Zanzíbar kwa mwaka wa masomo 2012-2013 Katika Mkopo huo wanafunzi 758 watakuwa wanasomea masomo ya Shahada ya kwanza, wanafunzi 40 Shahada ya Pili na Wanafunzi wawili wa masomo ya Shahada ya Tatu kutoka katika vyuo vilivyopo nchini Tanziania. Akitoa ufafanuzi huo leo Ofisini kwake Shangani Mjini Zanzibar Mwenyekiti wa Bodi hiyo Kombo Hassan Juma amesema idadi hiyo ni ongezeko kubwa kulinganisha na mwaka jana ambapo Jumla ya wanafuzi 209 ndiyo waliopata Mkopo kutoka kwa Bodi hiyo. Kombo amesema ongezeko hilo linatokana na kiwango cha Fedha kilichotengwa na Bodi hiyo kuongezeka ikilinganishwa na mwaka jana ambapo Jumla ya Shl. Bilioni 8 zitatumika mwaka huu kwa ajili ya wanafunzi hao. Amesema kiwango cha mwaka jana ilikuwa Shl.Bilioni 4 ambapo kwa mwaka huu kimepanda hadi kufikia Asilimia 100 na kufanya mwaka huu Shl.Bilioni 8 kutumika kwa kazi hiyo. Akielezea maombi yaliyotumwa na wanafunzi waliotaka kupatiwa Mkopo huo amesema walipokea fomu za wanafunzi 3,500 na hivyo kuwalazimu kuchunguza wenye vigezo stahiki ambapo waliamua kuwapatia wanafunzi hao 800 kulingana na kiwango cha fedha kilichopo. Aidha amefahamisha kuwa fani za masomo ya Sheria, Uongozi wa Umma na Uwalimu wa masomo ya Dini na Kiarabu ni masomo ambayo hayakupewa kipaumbele katika utolewaji wa Mikopo hiyo. Amesema Bodi imetoa vipaumbele vyake kwa wanafuzi hao kulingana na mahitaji ya Serikali ambapo fani za Masomo ya Sayansi na Watu wenye mahitaji maalumu ikiwemo Walemavu zimepewa umuhimu mkubwa. Alisema Walemavu wanne ni miongoni mwa watakaonufaika na Mkopo huo kati yao walemavu wawili ni wenye ulemavu waviungo na wawili Akili Kwa upende wake Mkurugenzi wa Bodi hiyo Idd Khamis Haji amesema Serikali inafanya Juhudi za kuhakikisha Vijana wenye sifa wanaendelea na kujiunga na masomo ya Elimu ya Juu kwa kadiri ya uwezo wa Fedha utakavyoruhusu. Aidha Idd amefahamisha njia za kufanikisha lengo kuwa ni pamoja na Walionufaika na Mikopo hiyo kuhakikisha wanarejesha Fedha hizo kwa wakati ili kutoa fursa kwa wengine kupata huduma hiyo. Njia nyingine ni pamoja na kuandaa Matembezi ya hisani, Chakula maalumu na kuomba misaada kutoka kwa Taasisi za ndani na nje ya Nchi ili kuhakikisha kila Mwanafunzi wa Zanzíbar mwenye sifa anafaidika na Mkopo wa Elimu ya Juu. Idd amewataka Watakaopata mikopo hiyo kwenda katika Ofisi ya Bodi hiyo ili kuweka Mikataba na kuongeza kuwa majina ya waliochaguliwa kupata Mkopo huo yatatangazwa punde kupitia Tovuti ya Bodi hiyo na Vyombo vya habari nchini. Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Zanzíbar ilianzishwa rasmi Julia 2011 kwa lengo la kusimamia upatikanaji wa Mikopo kwa wanafunzi wa Zanzíbar ambapo moja ya changamoto kubwa inayoikabili ni ongezeko kubwa la Wanafunzi wanaohitaji huduma hiyo ikilinganishwa na kiwango kidogo cha fedha.

No comments:

Translate