tangazo

Wednesday, July 11, 2012

DR SLAA AMJIBU WAZIRI NCHIMBI.

                                  Katibu mkuu wa chama cha demokrasia na maendeleo.(chadema)
                                                                  Waziri nchimbi


ATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dkt. Willibroad Slaa, amesema pamoja na madai waliyotoa kwa Serikali juu ya kuandaa mkakati wenye lengo la kuwateka, kuwadhuru baadhi ya viongozi wake kitaifa, hawapo tayari kuhojiwa na Jeshi la Polisi kama alivyoagiza Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dkt. Emmanuel Nchimbi.

Alisema msimamo huo unatokana na chama hicho kutokuwa na imani na jeshi hilo ambalo kwa nyakati tofauti, limeshindwa kushughulikia malalamiko ya chama hicho ambayo wamekuwa yakiyapeleka kwa masilahi ya Taifa.

Dkt. Slaa aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari siku moja baada ya Dkt. Nchimbi, kuliagiza Jeshi la Polisi kuwahoji baadhi ya viongozi wake waliodai Serikali imeanda mkakati huo ambao unaratibiwa na Usalama wa Taifa.

Mbali ya Dkt. Slaa, viongozi wengine waliodai kuandaliwa mkakati huo ambao Dkt. Nchimbi, aliagiza wahojiwe na polisi ni pamoja na aliyekuwa Mbunge wa Arusha Mjini, Bw. Godbress Lema na Mbunge wa Ubungo, Bw. John Mnyika.

“Tumechoshwa na tabia ya Jeshi la Polisi kupuuza malalamiko mbalimbali ambayo tunawapelekea juu ya kutoridhishwa na baadhi ya mambo yanayogusa masilahi ya Taifa hivyo hatupo tayari kuhojiwa wala hatuoni sababu ya kujipeleka vinginevyo tupo tayari kukamatwa,” alisisitiza Dkt. Slaa.

Alisema Kamati Kuu wa CHADEMA ambayo ilikutana jana, ililaani hatua ya viongozi wake kupokea vitisho ambavyo vinahatarisha usalama wa maisha yao.

Aliongeza kuwa, pamoja na vitisho hivyo, tayari amepokea simu kutoka kwa mtu mmoja aliyejitambulisha kuwa Ofisa wa Polisi kutaka akutane naye.

“Nilichomwambia ni kwamba, sina muda huo na sipo tayari kukutana naye wala mtu mwingine yeyote,” alisema Dkt. Slaa akipinga agizo la Dkt. Nchimbi, kutaka polisi iwahoji.

“Dkt. Nchimbi hakustahili kutoa agizo kama hili badala yake wao walipaswa kuichunguza Idara ya Usalama wa Taifa na Jeshi la Polisi ndiyo maana Wizara hii inapewa bajeti kubwa kwa ajili ya mambo kama haya.

“Wizara hii inatengewa fedha nyingi kwa ajili ya mambo kama haya hivyo lazima yachunguzwe kwa kina badala ya kutoa kauli zisizo na tija, umaaarufu wa chama chetu na sisi wenyewe hautokani na siasa bali ni kukubalika na wananchi si vinginevyo,” alisema Dkt. Slaa.

Katika hatua nyingine, chama hicho kimetangaza ratiba yake ya kujikita katika mikoa mitano siku 44 kwa ajili ya kujiimarisha na kuhamasisha wananchi kukiunga mkono.

Alisema mikutano hiyo imepewa jina la “Operesheni Sangara” chini ya kauli mbiu inayosema; “Hakuna kulala, hakuna kula, hakuna kunywa hadi kieleweke”.

Dkt. Slaa alisema miongoni mwa mikoa inayolengwa kwenye operesheni hiyo pamoja na Singida, Dodoma, Tabora, Shinyanga na watafika vijiji 4,000, kata 806 na majimbo 44, kwani lengo cha chama hicho ni kuongoza Serikali.

No comments:

Translate