tangazo

Monday, July 23, 2012

Wabunge Wamsafishia Zitto Njia Ya Urais 2015

 
NI JOSHUA NASSARI WA CHADEMA, DEO FILIKUNJOMBE WA CCM, WASEMA KIGOMA WAJIANDAE KUTOA RAIS
Anthony Kayanda, Kigoma na Fred Azzah Dar
IKIWA imebaki miaka mitatu kabla ya Uchaguzi Mkuu utakaofanyika nchini mwaka 2015, wabunge wawili vijana wamewataka wakazi wa Mkoa wa Kigoma kujiandaa kumpata kutoka eneo hilo.

Kauli za Wabunge hao zimekuja kipindi ambacho mchakato wa Katiba unaendelea huku kukiwa na uwezekano wa umri wakugombea urais kushuka hivyo kuwawezesha wanasiasa wengi vijana akiwamo Zitto, kugombea nafasi hiyo.

Wakizungumza katika tamasha kubwa lililokutanisha mamia ya wakazi wa Mkoa wa Kigoma, Deo Filikunjombe ambaye ni mbunge wa Ludewa (CCM), Joshua Nasari wa Arumeru Mashariki (Chadema) na Halima Mdee, Kawe (Chadema), walisema wanaamini Rais wa 2015 atakuwa Mbunge wa Kigoma kaskazini na ambaye ni mzaliwa wa mkoa huo.

Katika kauli yao hiyo, wabunge hao walisema Mbunge huyo ameonyesha umahiri mkubwa katika kusimamia mambo ya kitaifa bila upendeleo, jambo linalomfanya kujijengea umaarufu mkubwa ndani na nje ya nchi, hivyo kuonekana wazi kulibeba vema kundi la Vijana wa Taifa hili.

Akimzungumzia kuhusu rais ajaye kutoka Kigoma, Filikunjombe alisema kundi la vijana lazima liungane kuhakikisha kuwa linatoa viongozi watakaopigania maslahi yao na Taifa kwa jumla ili kuleta ukombozi wa kifikra na kimaendeleo kwa maslahi ya jamii.

"Lazima mtambue kuwa, Tanzania ni nchi yetu sisi wote na lazima vijana wote bila kujali itikadi zetu za kisiasa tunatakiwa kujipa moyo kwamba tunaweza kufanya makubwa katika kuleta maendeleo ya jamii katika nchi yetu," alisema Filikunjombe na kuongeza:

"Vijana wa Kigoma mnabahati ya kuwa na Wabunge wazuri na ninaamini miaka michache ijayo lazima mkoa huu utoe Rais wa Tanzania."

Huku akishangiliwa na umati mkubwa wa watu waliokusanyika katika uwanja wa Lake Tanganyika mjini hapa kuhudhuria tamasha hilo lililopambwa na wasanii nyota wa kizazi kipya kutoka Mkoa wa Kigoma, Filikunjombe alisema; "Zitto anastahili kuwa rais".

Mbunge huyo wa CCM ambaye katika siku za karibuni ameonekana kuwa mshirika mkubwa wa kisiasa wa Zitto na Chadema, alisema Zitto anafaa kuwa Rais kwani amefanikiwa kuwaunganisha watu na kuleta umoja miongoni mwao, jambo ambalo linadumisha umoja wa kitaifa.

No comments:

Translate