tangazo

Tuesday, July 10, 2012

Waliodaiwa kuhujumu miundombinu TTCL waachiwa

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imewaachia huru wafungwa watatu waliokuwa wakitumikia kifungo cha miaka mitatu jela kwa kuhujumu miundombinu ya mawasiliano ya Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL).

 Wafungwa hao walioachiwa ni Naclis Thomas, Charles na Mshamu Mbowela. Walihukumiwa kifungo cha miaka mitatu jela na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Agosti 29, mwaka jana baada ya kuwatika hatiani kwa makosa matatu ya kula njama, kuvuruga na kutumia isivyo halali mifumo ya mawasiliano ya TTCL.

Lakini, jana Mahakama Kuu iliwaachia huru baada ya kubaini kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilikosea katika kutoa adhabu, baada ya washtakiwa hao kukata rufaa wakipinga hukumu na adhabu hiyo. Akisoma hukumu hiyo jana, Jaji Dk Fauz Twaib, kwanza alitupilia mbali hoja za rufaa ya  warufani hao akisema hazina msingi na kwamba, mwenendo wa kesi ya msingi ulikuwa sawa.
Pia, Jaji Dk Twaib alisema anakubaliana na hoja za Wakili wa Serikali Mhina wakati wa usikilizaji wa rufaa hiyo kuwa, ushahidi uliowatia hatiani ulikuwa unajitosheleza na haukuhitaji ushahidi zaidi wa kuunga mkono, kama warufani walivyodai.

Hata hivyo, akihitimisha hukumu yake alikubaliana na hoja ya Wakili wa Serikali kuwa, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilikosea katika kutoa adhabu kwa kuwa adhabu waliyopewa warufani hao haikuwa sahihi. “Sikuona tatizo lililoharibu mwenendo wa kesi ya msingi kama warufani walivyodai.

Jambo ambalo lingeweza kuwasaidia ni kwamba Hakimu Fimbo (Sundi, aliyewahukumu adhabu hiyo) hakutaja kifungu cha sheria alichokitumia kutoa adhabu hiyo,” Jaji Dk Twaibu alisema na kuongeza:

“Hata hivyo, tatizo hilo linarekebishika chini ya kifungu cha 388 (1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA).”  Jaji Dk Twaib alisema kosa la kwanza na la pili ndiyo  makosa makubwa, ambayo adhabu yake ni faini ya Sh300,000 au kifungo cha miaka mitatu jela au vyote viwili kwa pamoja.

Kuhusu kosa la kwanza la kula njama, Jaji Dk Twaib alisema adhabu yake ni kifungo cha miaka saba jela, lakini akasema katia kutoa adhabu inabidi makosa makubwa pia yaangaliwe.

“Kisheria mahakama haina budi kuanza na adhabu ya faini, lakini hakimu alitoa adhabu ya kifungo moja kwa moja, hii si sahihi alipaswa aangalie kifungu cha faini kwanza,” alisema Jaji Dk Twalib na kuongeza:
“Hata kama aliona kifungu cha adhabu ya kifungo jela basi alipaswa aangalie kifungu kinachopunguza adhabu.” Alisema anakubaliana ilikuwa sahihi kuwatia hatiani kwa makosa hayo, lakini akaondoa adhabu ya kifungo itakayopelekea warufani kuachiliwa huru mara moja.

No comments:

Translate