tangazo

Friday, July 6, 2012

Chadema yaichimba Serikali kuhusu Taarifa za Iran kutumia Bendera ya Tanzania




CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeibebesha lawama Serikali kikidai ina kigugumizi kuhusu madai ya meli ya mafuta ya Iran kutumia bendera ya Tanzania ili kukwepa vikwazo vya kiuchumi vya kimataifa.
Naibu Katibu Mkuu wa Chadema (Zanzibar), Hamad Mussa Yussuf alisema kupitia taarifa kwa gazeti hili kwamba haoni sababu ya Serikali kujikanyaga katika jambo hilo.

“Tunashangaa kwa takribani muda wa juma moja sasa zimekuwapo taarifa katika vyombo vya habari kuhusu kampuni moja ya meli inayodaiwa kutoka Iran, inayojulikana kwa jina la NITC (National Iranian Tanker Company), inatumia Bendera ya Tanzania, isivyo kihalali,” alisema Yussuf.

Alielezea kwamba kitendo hicho ni kinyume kabisa na sheria za nchi na zile za kimataifa na kwamba ni jambo nyeti ambalo halipaswi kufanywa kama la mchezo lakini anashangaa Serikali inajikanyaga kutoa taarifa sahihi.

“Pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kukanusha taarifa hizo, Chadema kinaitaka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutoa taarifa kwa umma juu ya hatua ilizochukua kuchunguza madai hayo,” alisema.
Chadema imetoa shutuma hizo wakati Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe akisema kitendo hicho ni kosa kisheria, lakini akasema taarifa hiyo ni ngeni ila vyombo husika vitalichunguza.
Yussuf alisema kuwa ili Tanzania ijisafishe Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ilipaswa kushirikiana na Serikali ya Muungano kufanya uchunguzi wa haraka na kubaini msingi wa tuhuma hizo na kuchukua hatua.

Yussuf aliilaumu maofisa wa Serikali ya Zanzibar akisema siyo mara yao ya kwanza kufanya vitendo vya kizembe na kutoa mfano wa kashfa ya kuzama kwa meli ya Spice Islender.

Hofu ya Chadema alisema ni kwamba ina hofia “Tanzania itaonekana inaibeba na kuisaidia Iran kukwepa vikwazo ambavyo nchi hiyo inatishiwa na mataifa ya Magharibi, hasa Marekani na Umoja wa Ulaya.”
Yussuf alisema mataifa hayo makubwa hutumia mabavu na vitisho kuzichagulia baadhi ya nchi nyingine duniani, nini cha kufanya na rasilimali zake mathalani mzozo unaoendelea na Iran kuhusu urutubishaji wa madini ya urani.

“Si nia ya Chadema kuingia katika mgogoro wa Iran na Mataifa ya Magharibi hapa kupitia mjadala wa madai hayo yaliyoandikwa kwenye vyombo vya habari; lakini inatoa tamko kufuatia ukimya na kigugumizi cha Serikali,” alisema.

Chanzo cha sakata hili kinadaiwa kinatokana na Mbunge mmoja wa Marekani ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Masuala ya Nje, Howard Berman kuandika barua kwa Rais Jakaya Kikwete akimuarifu juu ya suala hilo la Meli za NIT kutuhumiwa kupeperusha Bendera za Tanzania.

No comments:

Translate